Baraza ya Majestic na Machinjioni kwa BamkweDl2a - Buluu Publishing, 24 juil. 2024 - 202 pages (swa) Kwa lugha nyepesi ya Kiswahili fasaha, Kiunguja, Ibrahim Mohammed Hussein, anasimuliya kwa uwazi na ujasiri mkubwa, yale yaliyomsibu baada ya kuuwawa Rais wa Kwanza wa iliyokuwa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar, na Mwenyekiti wa Kwanza wa Baraza la Mapinduzi, Sheikh Abeid Amani Karume. Tukio hilo la siku ya Ijumaa, tarehe 7 Aprili 1972, liliigubika nchi katika giza zito na kuzusha hamkani ya nguo chanika. Maisha Visiwani yakawa sio shwari tena. Kamatakamata ikawa ndio kilio kilichosikisika mitaani. Mwandishi wa kitabu hichi nae pia akanaswa ndani ya mtego wa panya, ulioingiza waliokuwemo na wasiokuwemo. Kilichomponza ni u-Ahlil Barza wake na Baraza ya Majestic, iliyokuwa katikati ya Mji Mkuu wa Zanzibar, aliyokuwa akijipumzisha kwa soga na maskhara na ahlil barza wenzake. Mithili ya chozi jichoni, tone la wino wa kalamu ya mwandishi, linasononeka kwa kuyanukuu madhila yaliyomkumba na kupelekea kunyang’anywa utu wake na hadhi yake kama binadamu. Mwili wake, kama wa madhulumu wenzake, uligeuzwa kama ngoma kucharazwa kwa vyuma na magongo ya mipera na milimau. Maisha yakawa hayana stara. Utupu wake kama ule wa wenzake haukutafautishwa na wa mnyama. Wote walilazimishwa kufanya haja zote mbele ya hadhara wakati wengine wakisubiri zamu zao. Ladha na utamu wa lugha aliyoitumia mwandishi kuielezea kadhia yake, yenye kusisimua na kuhuzunisha sana, inamfanya msomaji kuwa na raghba ya kukisoma kitabu bila ya kusita. Kila ukurasa unamsogeza karibu na pazia zito lililogubikwa, kwa miaka nenda miaka rudi, na mengi nyuma yake yasiyoweza kutarajiwa na hata kufikirika katika mazingira ya maisha na malezi ya Kizanzibari. Mwenye kuifahamu Zanzibar iliyokuwa imejengeka katika misingi ya dini ya Kiislamu, Imani, Utu na Ubinaadamu atapigwa na bumbuwazi kuyasoma yaliyokuwa yakijiri nyuma ya lango kuu la Jela ya Kiinua Miguu, hususan upande ule maarufu wa Kwa Bamkwe, uliokuwa kama Milki moja ya mungu Mtu, ambae wafuasi wake nao wakijiona kama ndio kina Munkar na Nakir wa humo ndani. Majahil waliotakabar hadi kufikia mpaka kiongozi wao mkuu, Mandera, kuthubutu kuwaambia madhulumu wake kwamba « huko nje Mungu ndiye mwenye kutowa rizki » lakini kule ndani, kwenye milki yake, ni « yeye mwenye kutowa rizki ». Ndani ya Jumba la Maafa, mwandishi anampitisha msomaji wake katika kuta na vichochoro vya mateso yaliyokithiri na watesaji waliofurutu ada kwa ukatili wao, mithili ya vikosi thakili vilivyokuwa vikitajika duniani, Gestapo (Ujerumani ya Aldof Hitler) na Tonton Macoutes (Haiti ya Duvallier). Kuta zilizosheheni sauti za vilio vya idhilali na mateso. Kuta zilizoyaona maafa mengi ya madhulumu waliotolewa roho zao mbichi au kutiwa vilema vya maisha vya kimwili na kiakili kwa kulazimishwa kukiri makosa wasiyoyajuwa. Mwandishi kama madhulumu wenzake wengine hakuwahi kupata uaidhi, ushauri wa kisaikolojia, baada ya kutoka jela. Jitihada zake za kuyaeleza yaliyomsibu na kumkwaza rohoni kupitia kitabu hichi, ni hatua moja kubwa muhimu katika harakati zake za kuitibu nafsi yake. (fre) Ibrahim Mohammed Hussein fut arrêté le 11 avril 1972, dans le sillage de l'assassinat du Président Karume à Zanzibar, à la suite d’accusations infondées le liant à cet attentat comme "traître à la révolution". Initialement condamné à mort, il passa plus de six années en prison, où il endura des tortures inhumaines, dans la partie de la prison de Kiinua Miguu célèbrement connue de "Kwa Bamkwe", qu'il qualifie "d'abattoir". À la différence de l'écrivain swahili Adam Shafi, qui dans son ouvrage "Haini" a choisi une approche allégorique et l'usage de pseudonymes pour relater les sévices qu'il a subis et les violations des droits humains à Zanzibar, Hussein opte pour une narration directe et sans fard. Ce livre en swahili constitue une étape cruciale pour la vérité et la réconciliation sur l'île de Zanzibar après la révolution et représente, au moins sur le plan thérapeutique, une avancée vers la reconstruction des victimes de la vague d'arrestations arbitraires de l'époque. C'est aussi un témoignage précieux et une occasion de réflexion sur les violations des droits humains dans les prisons et les moyens à mettre en place pour les prévenir. |

